Waweza Kuishi na Yesu, lakini huwezi kuishi bila Yesu.Yohan 3:16


TWAWEZA KUIAMINI BIBLIA
Mabaharia waasi maarufu walioizamisha meli ya Kiingereza iliyoitwa Bounty waliishia kufanya makazi yao wakiwa pamoja na wanawake, wenyeji wa eneo lile katika kisiwa cha Pitcairn katika Bahari ya Pasifiki ya Kusini. Kundi lile lilikuwa mabaharia tisa wa Kiingereza, wanaume wa Kitahiti sita, wanawake wa Kitahiti kumi, na msichana wa miaka kumi na mitano. Mmojawapo wa mabaharia wale alivumbua namna ya kutonesha [kugeuza kuwa mvuke] alkoholi, na baada ya muda mfupi ulevi ukaliharibu koloni lile lililokuwa katika kisiwa kile. Ugomvi kati ya wanaume na wanawake ukageuka na kuwa wa kutumia nguvu.
Baada ya kupita muda fulani mmoja tu kati ya wanaume wale wa kwanza waliofika mle kisiwani ndiye alibaki kuwa hai. Lakini mtu huyo, Alexander Smith, alikuwa ameigundua Biblia katika mojawapo la makasha yaliyochukuliwa kutoka katika ile meli. Alianza kuisoma na kuwafundisha wengine juu ya kile ilichosema. Alipofanya hivyo maisha yake yeye mwenyewe yakabadilika na hatimaye maisha ya wote waliokuwa katika kisiwa kile.
Wakazi wa kisiwa kile walikuwa wametengwa na ulimwengu wa nje mpaka ilipowasili meli ya Kimarekani iliyoitwa Topaz katika mwaka wa 1808. Wafanyakazi katika meli hiyo wakakikuta kisiwa kile kikiwa na jumuia inayokua na kusitawi, bila ya kuwa na pombe kali (wiski), gereza, wala uhalifu. Biblia ilikuwa imekigeuza kisiwa kile kutoka jehanamu ya duniani kwenda katika kielelezo cha vile Mungu atakavyo ulimwengu huu uwe. Na mpaka leo hii kinaendelea kuwa katika hali hiyo.
Je, hivi Mungu bado anaendelea kusema na watu kupitia katika kurasa hizo za Biblia? Bila shaka anafanya hivyo. Ninapoandika haya, naliangalia karatasi la majibu lililotumwa kwetu na mwanafunzi mmojawapo wa kozi zetu za Biblia. Maelezo chini yake yanasema hivi "Mimi nimo gerezani, niko katika orodha ya watu wanaostahili kunyongwa, nimehukumiwa kufa kwa kutenda kosa la jinai. Kabla ya kuchukua kozi hii ya Biblia, nilikuwa nimepotea lakini sasa ninacho kitu cha kutumainia tena nimeupata upendo mpya."
Biblia inao uwezo unaoweza kuyabadilisha kabisa maisha ya watu. Kwa kweli, watu wanapoanza kujifunza Biblia, maisha yao hubadilika kwa namna ya kuvutia sana.

1. Jinsi Mungu Anavyozungumza Nasi Kupitia Katika Biblia

Baada ya kumwumba Adamu na Hawa, yaani, yule mwanaume na mwanamke wa kwanza wa duniani, Mungu alizungumza nao uso kwa uso. Lakini Mungu alipokuja kuwatembelea baada ya wao kutenda dhambi, je, wale watu wawili walifanya nini?
"Mwanaume yule na mkewe wakasikia sauti ya BWANA Mungu alipokuwa akitembea mle bustanini wakati wa jua kupunga, nao WAKAJIFICHA ASIWAONE BWANA MUNGU katikati ya miti ya bustani." (Mwanza 3:8). 
Dhambi ilikata mawasiliano ya ana kwa ana kati ya mwanadamu na Mungu. Baada ya dhambi kuingia katika ulimwengu huu, je, Mungu aliwasilianaje na watu?
"Hakika Bwana Mwenyezi hafanyi kitu, bila kuwafunulia watumishi wake manabii nia yake." - Amosi 3:7.
Mungu hakutuacha sisi gizani kuhusu maisha haya tuliyo nayo na maana yake. Kupitia kwa manabii wake - yaani, watu wale aliowaita Mungu kuwa wanenaji na waandishi wake - wamefunua majibu yake kwa maswali makuu yahusuyo maisha yetu.

2. Ni Nani Aliyeiandika Biblia?

Manabii waliutoa ujumbe wa Mungu kwa kutumia sauti na kalamu zao katika kipindi chao walichoishi, na walipokufa, maandiko yao yaliendelea kuwapo baada yao. Kisha ujumbe huo wa manabii ulikusanywa pamoja chini ya uongozi wake Mungu, na kuwekwa katika kitabu tunachokiita Biblia.
Lakini maandiko yao hayo yanaaminika kwa kiasi gani?
"Zaidi ya hayo, lakini kumbukeni kwamba hakuna mtu ye yote awezaye kufafanua mwenyewe unabii ulio katika Maandiko Matakatifu. Maana hakuna ujumbe wa kiunabii unaotokana na matakwa ya binadamu bali watu walitoa unabii wakiongozwa na Roho Mtakatifu" (2 Petro 1:20,21).
Waandishi wa Biblia waliandika si kwa kufuata mapenzi au tamaa yao, bali kama walivyoongozwa au kuvuviwa na Roho wa Mungu. Biblia ni kitabu cha Mungu!
Katika Biblia hiyo Mungu hutuambia habari zake Mwenyewe, tena hutufunulia makusudi yake aliyo nayo kwa ajili ya wanadamu. Inaonyesha mtazamo wa Mungu kwa mambo yale yaliyopita, kisha inatufunulia mambo ya mbele, ikitueleza jinsi tatizo la uovu litakavyotatuliwa mwishoni na jinsi amani itakavyokuja katika dunia yetu.
Je, hivi Biblia yote ni ujumbe utokao kwa Mungu?
"Maandiko yote, Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu, na yanafaa kuonya, kusahihisha makosa yao, na kuwaongoza, katika kufundishia ukweli, mtu wa Mungu awe mkamilifu na tayari kabisa kufanya kila kazi njema, waishi maisha adilifu" - (2 Timotheo 3:16,17).
Biblia Takatifu huyabadilisha kabisa maisha ya wanadamu kwa sababu Biblia "yote" ina "pumzi ya Mungu," ni hati iliyovuviwa, ni kitabu cha Mungu. Manabii walisimulia kile walichokiona na kukisikia kwa kutumia lugha ya wanadamu, lakini ujumbe wao ulitoka moja kwa moja kwa Mungu. Kwa hiyo, ukitaka kujua maisha haya yana maana gani, soma Maandiko Matakatifu. Kuisoma Biblia kutayabadilisha kabisa maisha yako. Kadiri unavyozidi kuisoma kwa maombi, ndivyo utakavyozidi kupata amani moyoni mwako.
Roho Mtakatifu yule yule aliyewavuvia manabii kuandika, Biblia hiyo, atayafanya mafundisho ya Biblia, injili yake, ifae kuyabadilisha kabisa maisha yako ukimwalika Roho kuwapo wakati unapoisoma hiyo Biblia.

3. Umoja wa Biblia

Kwa kweli Biblia ni maktaba ya vitabu 66. vitabu 39 vya Agano la Kale viliandikwa kuanzia karibu na mwaka wa 1450 K.K hadi 400 K.K, Vitabu 27 vya Agano Jipya viliandikwa kati ya mwaka wa 50 B.K na mwaka wa 100 B.K.
Nabii Musa alianza kuandika vitabu vitano vya kwanza wakati fulani kabla ya mwaka wa 1400 K.K. Mtume Yohana alikiandika kitabu cha mwisho cha Biblia, yaani, kitabu cha Ufunuo, karibu na mwaka wa 95 B.K. Katika kipindi cha miaka 1,500 kati ya kuandikwa kitabu cha kwanza na cha mwisho cha Biblia, walau watu wengine wapatao 38 waliovuviwa walitoa mchango wao. Wengine walikuwa wafanya biashara, wengine wachungaji wa kondoo, wengine wavuvi, wengine askari, matabibu, wahubiri, wafalme - wanadamu toka katika tabaka zote za maisha. Mara nyingi waliishi katika utamaduni na falsafa vilivyohitilafiana.
Lakini hapa ndipo yalipo maajabu ya maajabu yote: Vitabu hivyo 66 vya Biblia pamoja na sura zake 1,189 zenye idadi ya mafungu 31,173 vikiwekwa pamoja, tunaona umoja na mwafaka katika ujumbe vinaoutoa.
Hebu na tuseme kwamba mtu mmoja anagonga mlangoni pako, halafu anapokaribishwa ndani, anaweka kipande cha marumaru chenye umbo la ajabu juu ya sakafu ya chumba chako cha kuongea, halafu anaondoka bila kusema neno lo lote. Wageni wengine wanamfuata, mmoja baada ya mwingine, mpaka takribani watu 40 wanaweka kila mmoja kipande chake cha marumaru mahali pake.
Wa mwisho anapokwenda zake, kwa mshangao wewe unaona jengo zuri limesimama mbele yako. Ndipo wewe unajifunza kwamba sehemu kubwa ya "mafundi hao wanachonga mawe" hawajawahi kuonana kamwe, wakiwa wamekuja, kama walivyofanya, kutoka Amerika ya Kusini, China, Urusi, Afrika na sehemu nyingine za ulimwengu.
Je, wewe ungeamua nini? Ya kwamba mtu fulani alipanga umbo hilo lililojengwa kwa mawe ya kuchonga naye alimtumia kila mtu vipimo sahihi kutokana na kipande chake kile kimoja cha marumaru.
Biblia nzima inatoa ujumbe mmoja unaoshikamana - sawasawa tu na lile jengo la mawe yaliyochongwa ya marumaru. Mtu fulani mmoja mwenye akili alipanga yote hayo, yaani, ni akili za Mungu. Umoja wa kushangaza wa Maandiko Matakatifu unatoa ushahidi wake kwamba ingawa ni wanadamu walioyaandika mawazo yale, yalikuwa yamevuviwa naMungu.

4. Waweza Kuiamini Biblia

1. Kuhifadhiwa kwa Biblia ni jambo la ajabu sana. Maandiko yote ya awali ya Biblia yalinukuliwa kwa mkono - muda mrefu kabla ya kuwako
mitambo ya kuchapisha vitabu. Waandishi wale walitayarisha nakala za maandiko ya mkono ya asilia na kuzitawanya. Maelfu ya nakala kama hizo za maandiko ya mkono au sehemu zake bado ziko mpaka sasa.
Maandiko ya mkono ya Kiebrania yanayorudi nyuma hadi ule mwaka wa 150 mpaka 200 kabla ya Kristo yalipatikana karibu na Bahari ya Chumvi mnamo mwaka 1947. Ni jambo la kushangaza sana kwamba magombo hayo mawili yenye umri wa miaka elfu mbili yanazo kweli zile zile tunazozikuta katika Agano la Kale la Biblia zinazochapishwa siku hizi. Huu ni ushahidi wenye nguvu unaoonyesha jinsi Neno la Mungu linavyoaminika.
Mitume waliandika kwanza sehemu kubwa ya Agano Jipya kama nyaraka walizozituma kwa makanisa ya Kikristo yaliyoanzishwa baada ya kifo na ufufuo wake Kristo. Zaidi ya maandiko ya mkono 4,500 ya Agano Jipya lote au sehemu yake yanapatikana katika nyumba za Makumbusho na maktaba za Ulaya na Amerika. Baadhi yake yanakwenda nyuma hadi karne ile ya pili. Kuyalinganisha maandiko hayo ya mkono ya awali na biblia ya siku hizi, twaweza kuona kwa urahisi kwamba kwa kawaida Agano Jipya limeendelea pia kubaki bila mabadiliko yo yote tangu lilipoandikwa kwa mara ya kwanza.
Siku hizi Biblia au sehemu zake zimetafsiriwa katika lugha zaidi ya 2,060 na (dialects). Ni kitabu kinachouzwa sana ulimwengu: zaidi ya Biblia milioni 150 na sehemu za Biblia huuzwa kila mwaka.
2. Usahihi wa Biblia kihistoria ni wa kushangaza sana. Uvumbuzi mwingi wa elimu ya mambo ya kale (akiolojia) umethibitisha kwa namna ya kuvutia sana usahihi wa Biblia. Wanahistoria wamevigundua vibao vya udongo wa mfinyanzi pamoja na majengo ya kumbukumbu ya mawe ambayo yameonyesha majina, mahali, na matukio yaliyojulikana kuhusu siku za nyuma kutokana na Biblia tu.
Kwa mfano, kulingana na Mwanzo 11:31, Ibrahimu na familia yake "wakatoka wote katika Uru... waende katika nchi ya Kanaani." Kwa kuwa ni Biblia peke yake iliyosema juu ya Uru, mabingwa fulani wa Biblia walisema kwamba mji kama huo ulikuwa haujapata kuwako kamwe. Ndipo wachimbaji wa mambo ya kale wakagundua mnara wa hekalu katika nchi ya Iraki Kusini ukiwa na kwenye msingi wake iliyoandikwa katika maandishi ya kikabari yaliyokuwa na jina la Uru. Ugunduzi wa baadaye ulionyesha kwamba Uru ulikuwa ni mji mkuu ambao ulikuwa unasitawi wenye ustaarabu wa hali ya juu uliokuwa umefikiwa. Sura ya mji ule ilikuwa imesahaulika ni Biblia peke yake iliyolihifadhi jina lake - mpaka pale koleo ya mwanaakiolojia mmoja ilipouthibitisha ukweli wa kuwako kwake. Na huo Uru ni mmoja tu miongoni mwa mifano mingi ya akiolojia inavyothibitisha usahihi wa Biblia.
3. Kutimia kwa usahihi kabisa kwa utabiri wa Biblia hukuonyesha wewe kwamba unaweza kuitegemea Biblia. Maandiko hayo yana utabiri mwingi wa kushangaza sana wa matukio ya siku za usomi ambayo hivi sasa yanaendelea kutimia mbele ya macho yetu. Tutauchunguza baadhi ya unabii huo wa kusisimua katika masomo ya mbele.

5. Jinsi Ya Kuielewa Biblia

Unapolichunguza Neno la Mungu, weka kanuni hizi mawazoni mwako:
1. Jifunze Biblia ukiwa na moyo wa maombi. Ukiyaendea Maandiko Matakatifu kwa moyo na mawazo yaliyofunguliwa kwa maombi, yatageuka na kuwa mawasiliano kati yako na Yesu (Yohana 16:13-14).
2. Soma Biblia kila siku. Kujifunza Biblia kila siku ni ufunguo wa kupata nguvu katika maisha yetu, ni kukutana na mawazo ya Mungu (Warumi 1:16).
3. Unapoisoma, iache Biblia ijieleze yenyewe. Uliza: mwandishi huyu wa Biblia alikusudia kusema nini? Kwa kuzingatia kile limaanishacho fungu hilo, twaweza kuitumia kwa akili katika maisha yetu ya leo hii.
4. Soma Biblia kwa kufuata somo. Linganisha andiko na andiko. Yesu alitumia mbinu hii kuthibitisha kwamba yeye alikuwa ndiye Masihi:
"Akaanza kutoka Musa na Manabii wote, akawaeleza katika maandiko yote mambo yaliyomhusu yeye mwenyewe."
5. Jifunze Biblia ili kupokea uwezo wa kuishi kwa ajili ya Kristo. Neno la Mungu limeelezwa katika Waebrania 4:12 kama upanga mkali ukatao kuwili. Ni zaidi ya maneno tu yaliyo juu ya ukurasa, ni silaha iliyo hai mikononi mwetu ya kupigia na kuyaondolea mbali majaribu yale yanayotushawishi kutenda dhambi.
6. Sikiliza Mungu anapozungumza nawe kupitia katika Neno lake. Endapo mtu anataka kuujua ukweli wa Bilbia juu ya somo fulani, basi, ni lazima awe tayari kufuata yale inayofundisha (Yohana 7:17), sio yale anayofikiri mtu fulani, au yale yanayokaziwa na fundisho lolote la kanisa lake.

6. Biblia Yaweza Kubadilisha Maisha Yako

"Kuyafafanua maneno yako [Mungu] kwatia nuru, kunampa ufahamu mjinga" - (Zaburi 119:130).
Kujifunza Biblia kutauimarisha "ufahamu" wako, kutakupa nguvu ya kuyashinda mazoea yale yaletayo madhara, na kukuwezesha kukua kimwili, kiakili, kimaadili na kiroho.
Biblia inazungumza na moyo. Inashughulika na mambo yale yanayowapata wanadamu katika maisha yao - yaani, upendo, ndoa, uzazi na kifo. Inaliponya jeraha lenye kina kirefu sana katika tabia ya mwanadamu, pamoja na dhambi na taabu inayotokana nayo.
Neno la Mungu si kitabu cha jamii moja, kizazi kimoja, taifa moja, au utamaduni mmoja. Japokuwa liliandikwa katika nchi ya Masharikiya kati, linawavutia pia wanaume na wanawake wa Magharibi. Linaingia katika nyumba za wanyonge na katika majumba makubwa ya matajiri. Watoto wanazipenda hadithi zake zinazosisimua. Mashujaa wake wanawavutia sana vijana. Wagonjwa, wanaoishi katika hali ya upweke, na wazee wanagundua ndani yake faraja na tumaini la kuwa na maisha bora.
Kwa kuwa Mungu anafanya kazi yake kupitia katika Biblia, basi, inao uwezo mkubwa. Inaivunjavunja hata mioyo iliyofanywa migumu dhidi ya hisia zote za kibinadamu, inailainisha na kuijaza na upendo. Tumeona Biblia ikimbadilisha haramia wa zamani na mvuta bangi na kumfanya mhubiri aliye motomoto. Tumeona Biblia ikimbadilisha mwongo na mdanganyaji na kumfanya kuwa mwalimu mwaminifu na mwenye kuheshimika. Tumeona kitabu hicho kikiwanyakua watu wakiwa karibu na kujiua wenyewe na kuwapa tumaini la kuanza maisha upya. Biblia inaamsha upendo miongoni mwa maadui. Inawafanya wenye majivuno kuwa wanyenyekevu, na wachoyo kuwa wakarimu. Biblia inatutia nguvu tunapokuwa dhaifu, inatuchangamsha tunapokuwa katika hali ya kukata tamaa, inatufariji tunapokuwa na huzuni, inatuongoza tunapochoka sana. Inatuonyesha jinsi ya kuishi kwa ujasiri na jinsi ya kufa bila hofu.
Kitabu hicho cha Mungu, yaani, Biblia kinaweza kuyabadilisha maisha yako! Utagundua hivyo kwa dhahiri zaidi na zaidi, kadiri unavyoendelea kujifunza miongozo hii ya GUNDUA.
Kwa nini Biblia hiyo iliandikwa kwa ajili yetu? Yesu anatoa jibu: "Lakini hizi [kweli za Biblia] zimeandikwa; ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini muwe na uzima kwa jina lake" - (Yohana 20:31).
Sababu kuu kuliko zote kwa nini sisi tunapaswa kuyafahamu Maandiko Matakatifu ni kwamba yamejaa picha zinazomfunua Yesu Kristo na kutuhakikishia sisi uzima wa milele. Kwa kumtazama Kristo katika Biblia nzima, tunabadilika na kufanana naye zaidi. Basi, kwa nini wewe usianze sasa kugundua uwezo huo wa Neno la Mungu uwezao kukufanya wewe kufanana zaidi na Yesu?

No comments:

Post a Comment